Wednesday, November 8, 2017

CHIMBUKO LA KISWAHILI

Chimbuko la kiswahili

Bismillahi (tamko la kuashiria kuanza jambo jema kwa jina la Mwenyezi Mungu)! Yafuatayo ni maelezo ya Kamusi la Kiswahili Fasaha, chapisho la Baraza la Kiswahili la Zanzibar, mwaka 2010.
“Kiswahili, kama zilivyo lugha zote duniani kilianza kusemwa na kundi la watu waliojinasibu kwa sifa za kijamii zilizowaunganisha na kisha kusambaa katika makabila mbalimbali ya mwambao wa Afrika Mashariki, kuanzia Barawa hadi Sofala pamoja na visiwa vilivyo karibu na mwambao huo.
“Kumekuwa na hali ya kutafautiana miongoni mwa wataalamu juu ya chimbuko la Kiswahili. Nadharia kadhaa zimetolewa katika kujaribu kubainisha asili ya lugha ya Kiswahili.

1.“Nadharia mojawapo ni ile inayotoa hoja kuthibitisha kuwa Kiswahili ni Krioli (lugha ya awaliya wazungumzaji iliyoibuka kutokana na mchanganyiko wa lugha nyingi) iliyoibuka kutokana na mwingiliano wa lugha fulani za Kibantu na Kiarabu.

2.“Nadharia nyingine ni ile inayodai kuwa Kiswahili ni Kiarabu.

3.Nadharia ya tatu inatoa hoja kuwa Kiswahili ni mojawapo ya lugha za Kibantu.
“Nadharia hii ya tatu imekubalika miongoni mwa wataalamu kwa vile hoja zake zimethibitishwa kitaalamu kwa kutumia misingi ya isimu*”
*Isimu ni tawi la taaluma inayochunguza na kuchambua mifumo na miundo ya lugha, sayansi ya lugha. Ni mtaala ambao huchunguza lugha kama mfumo wa mawasiliano ya wanadamu. Huandama mikabala mbalimbali na tofautitofauti ya kisayansi na hivyo huwa na usayansi ndani yake.
(i) Utoshelevu wa kiutenzi: Isimu hudhihirisha uteuzi wa kiunzi fulani (kimoja maalumu) cha kiuchunguzi na wala si kingine.
(ii) Utoshelevu wa kiuchunguzi: Mwanaisimu hueleza yote yanayoonekana katika kongoo (mkusanyiko wa matini tofautitofauti zenye madhumuni maalumu ya kiutafiti) lililochaguliwa bila ya upungufu au mapuuza.
(iii) Utoshelevu wa kiufafanuzi: Isimu hushadidia (kitendo cha kutaka jambo lifanywe kwa hali yoyote) ufafanuzi wa viwango vyote: fonetiki, fonolojia, mofolojia, pragmatiki, semantiki na sintaksia.
(iv) Uchechefu (uchache, udogo): Tofauti zote za kongoo na lugha husika huwekwa dhahiri.
(v) Uwazi: Mawanda (eneo ambalo akili ya mtu yaweza kuwa na ufahamu nalo) ya sheria zinazohusika katika ufafanuzi wa lugha yapaswa kuwa wazi na yasiwe na utata wala kupingana.
Matawi ya Isimu: Isimu historia, isimu fafanuzi, isimu linganishi, isimu jamii, isimu tumizi, isimu Kiafrika, isimu falsafa, isimu tiba, isimu nafsia na isimu kompyuta. (Kamusi ya Karne ya 21 ukurasa
Kama kawaida naendelea kukukaribisha utembelee blog yangu Mara kwa Mara ili kupata mambo mengine mengi na mazur zaidi kisanue na kwa mshikaji apate kujua. Sayansinaafya.blogspot.com.
AY director

No comments:

Post a Comment